Mshindi wa kwanza kwa upande wanawake wa mbio za baiskeli za Acacia tufanikiwe pamoja cycle Challange 2016,Martha Anthony akiwa amenyanyua juu kikombe mara baada ya kukabidhiwa na mgeni rasmi.
Mkuu wa kitengo cha biashara katika Mgodi wa Buzwagi,Jackson Kanumba akikabidhi zawadi kwa mshiriki wa mbio hizo Ashiraf.
Mshiriki Ashraf ambaye amekua akishiriki mashindano mbalimbali ya baiskeli ,akipongezwa na Meneja Mkuu wa Mgodi wa Buzwagi,Asa Mwaipopo.
Na Dixon Busagaga wa Michuzi Blog.
FAINALI ya mashindano ya mbio za baiskeli zijulikanazo kama “Acacia Tufanikiwe Pamoja Cycle challange 2016 zinazoandaliwa na chama cha mchezo wa mbio za baiskeli (CHABATA) na kudhaminiwa na kampuni ya kuchimba Madini ya Acacia zimemalizika mjini Kahama huku mwendesha baiskeli Seni Konda akiweka rekodi ya kushinda mbio hizo kwa kutumia saa 4:15:07 .
Konda mkazi wa mkoa wa Shinyanga amefanikiwa kushika nafasi hiyo baada ya kuwashinda wapinzani wake Makoja Hamis aliyemaliza nafasi ya pili na Hamis Clement aliyemaliza nafasi ya tatu huku wakifuatiwa na waendesha baiskeli zaidi ya 150 walioshiriki mbio hizo kutoka mikoa sita ya kanda ya ziwa.
Kwa upande wa wanawake ,mwendesha baiskeli,Martha Anthony kutoka mkoani Mwanza amefanikiwa kutetea ubingwa wake akimaliza wa kwanza huku akiwashinda washindani wake,Salma William aliyeshika nafasi ya pili na Elizabeth Clement aliyeshika nafasi ya tatu.
Mshindi wa kwanza kwa upande wa wanaume ,Seni Konda amejinyakulia kitita cha sh Mil 1.5 ,mshindi wa pili Makoja Hamis akijinyakulia kiasi cha sh Mil moja huku mshindi wa tatu ,Hamis Clement akiambulia kiasi cha sh 700,000.
Upande wan wanawake mshindi wa kwanza Martha Anhtony amejinyakulia kiasi cha sh Mil 1.2,mshindi wa pili Salma William akipata sh 800,000 huku mshindi wa tatu ,Elizabeth Clement akipata sh 600,000.
Akizungumza kabla ya kukabidhi zawadi kwa washindi wa mbio hizo mgeni rasmi naibu waziri wa habari, utamaduni, Sanaa na michezo Anastazia Wambura amesema michezo ni ajira na afya ambapo pia amewataka wachezaji kutotumia madawa ya kusisimua misuri kwa kuwa kitendo hicho ni kinyume cha taratibu za michezo na atakayebainika atachukuliwa hatua kali za kisheria.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Baiskeli cha Tanzania (CHABATA) Jacx Mhagama alisema CHABATA na kampuni ya madini ya ACACIA wamesaini mkataba wa udhamini wa mashindano hayo kwa muda wa miaka mitatu kuanzia 2014 mpaka 2016.
“Kipindi hiki cha miaka mitatu kimekuwa na mengi kiutendaji na kimahusiano kwetu sote CHABATA na ACACIA. lakini kwetu imekuwa ni kipindi chenye chenye changamoto zenye kutukomaza na kutujenga. Hivyo tumevuna tuliyoyategemea na ziada pia.”alisema Mhagama.
“ACACIA ni kampuni yenye machimbo ya madini kwenye eneo hili la kanda ya Ziwa, lakini wameonyesha upendo na uzalendo mkubwa hata kwa Taifa. Pamoja na kujishughulisha na michezo kwenye eneo hili la kanda ya ziwa, wameenda juu Zaidi kufikia taifa kwa kuifadhili timu yetu ya Taifa ya Baiskeli kwenye mashindano ya Ubingwa wa Afrika mwaka jana 2015, yaliyofanyika huko Petermarizburg nchini Afrika ya Kusinu.”aliongeza Mhagama.
Mwisho.